Plus 255 Studios

Plus 255 Studios
Home » » Werema, Kafulila Nitamkata kichwa

Werema, Kafulila Nitamkata kichwa


Dodoma. Mvutano kati ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema na Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila umechukua sura mpya baada ya mwanasheria huyo kugoma kupatanishwa huku akitishia ‘kumshughulikia’ mbunge huyo.
Ugomvi baina yao uliendelea jana asubuhi nje ya Ukumbi wa Bunge muda mfupi baada ya Naibu Spika, Job Ndugai kuahirisha kikao cha Bunge hadi leo.
Licha ya Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Azzan Zungu kumwita Jaji Werema na Kafulila akiwataka kupeana mikono kama ishara ya kuzika tofauti zao, Jaji Werema alikataa na nusura amvamie mbunge huyo.
Juzi asubuhi baada ya Zungu kuahirisha kikao cha Bunge, muda mfupi baada ya Jaji Werema na Kafulila kurushiana maneno bungeni, mwanasheria huyo alitaka kumtia adabu Kafulila kwa kumwita mwizi.
Kafulila alimwita Jaji Werema mwizi akijibu mapigo baada ya awali kuitwa tumbili na mwanasheria huyo.
Ilivyokuwa jana
Wakati akizungumza na gazeti la mwananchi mara baada ya Bunge kuahirishwa jana, Jaji Werema alikutana uso kwa uso na Kafulila katika Viwanja vya Bunge na kuanza kumlalamikia mbunge huyo kwa kitendo chake cha kumwita mwizi.
“Unamuona huyo jana (juzi), aliniita mimi mwizi. Yaani mtu mzima kama mimi naitwa mwizi, kwa kweli sikupendezwa kabisa na kauli yake,” alisema Jaji Werema huku akimfuata Kafulila ambaye alitembea harakaharaka kumkwepa mwanasheria huyo.
Jaji Werema alisema juzi alishikwa na jazba baada ya kuitwa mwizi lakini akasema hakuwa na nia ya kumpiga ndani ya Ukumbi wa Bunge.
Wakati Jaji Werema akiendelea kumlalamikia Kafulila, alitokea Zungu na kumtaka mwanasheria huyo kumsamehe mbunge huyo... “Mheshimiwa naomba mpeane tu mikono kama ishara ya kusameheana, yale mambo ya jana (juzi) yamekwisha.”
Lakini badala ya kukubaliana na ombi la Zungu, Jaji Werema alihamaki huku akitaka tena kumvamia Kafulila... “Mimi nakwambia Kafulila nitakukata kichwa, we subiri tu labda ukiniomba msamaha.”
Kafulila naye alijibu mapigo... “Huwezi kunikata kichwa Werema, huwezi, yaani uniue, hapana huwezi tena nakwambia huwezi.”

0 comments:

Post a Comment