Plus 255 Studios

Plus 255 Studios
Home » » Wasomi watoa tahadhari majadiliano ya JK, wapinzani

Wasomi watoa tahadhari majadiliano ya JK, wapinzani

Dar es Salaam. Wasomi wameonyesha wasiwasi wao juu ya mazungumzo kati ya Rais Jakaya Kikwete na vyama vya siasa vya upinzani vyenye wabunge, kuhusu tofauti zilizojitokeza katika Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
Wasomi hao licha ya kuunga mkono mazungumzo, wamesema wanasiasa wana kawaida ya kuwa na agenda za siri jambo ambalo baadaye huzusha tena mzozo, huku wakirejea kwamba si mara ya kwanza kwa Rais Kikwete kufanya mkutano wa aina hiyo.
Kauli hizo zimetokana na Rais Kikwete kukutana na viongozi wa vyama vya siasa; CCM, Chadema, CUF, NCCR Mageuzi, TLP na UDP kukubaliana kuweka pembeni tofauti za kiitikadi na kutanguliza masilahi ya taifa katika mchakato wa kuandikwa kwa Katiba Mpya.
Mhadhiri Mstaafu wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Dk Azavery Lwaitama alisema uamuzi wa Rais Kikwete ni mzuri lakini unaweza ukawa umechezwa kwa karata ya kisiasa.
Alifafanua, “Inaweza kuwa karata ya kisiasa kwa sababu bado Bunge lina wabunge wengi wa CCM, pia marekebisho yatasimamiwa na Waziri wa Katiba na Sheria, (Mathias Chikawe) sijui kutakuwa na jipya gani.”
Lwaitama alisema ili mambo yaende sawa, Rais Kikwete anatakiwa kuhakikisha kuwa marekebisho hayo yatakayofanywa nje ya Bunge, hayabadilishwi tena bungeni. “Ahakikishe kuwa wabunge wanapitisha tu yale ambayo yamerekebishwa nje ya Bunge.”
Naye Profesa Gaudence Mpangala wa UDSM alisema: “Tutajua kama hili jambo limetulia ama la, kama Bunge likipitisha mapendekezo mapya, kama ikiwa hivyo mambo yatakwenda vizuri.”
Hata hivyo, Profesa Mpangala alionyesha wasiwasi wake kama wabunge wataamua kuyapinga mabadiliko hayo, huku akishauri itumike njia ambayo itawafanya wabunge kukubaliana na kile kilichojadiliwa nje ya Bunge.
Alisema Katiba nzuri ni lazima itokane na mwafaka wa pamoja na kwamba nia ya Rais Kikwete inapaswa kuendelezwa hadi bungeni.
Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Bashiru Ally alisema: “Siku zote mtu asiyejua anapokwenda hawezi kupotea njia, mchakato wa Katiba Mpya una mgongano wa mtazamo kuna maswali mengi kuhusu mchakato huu kuwa wa kisiasa na kisheria.
Alisema kuwa mchakato huo sasa haujulikani unaendeshwa kwa masilahi ya nani, kwa sababu kila malalamiko mengi yanayotolewa yamebebwa na vyama vya siasa.
“Tupo njiapanda, binafsi sina imani kubwa na mchakato huu, vyama vimeweka masilahi yao zaidi mbele,” alisema Bashiru.

0 comments:

Post a Comment