Plus 255 Studios

Plus 255 Studios
Home » » Viongozi wa Ukawa wauteka Mkutano Mkuu Chadema

Viongozi wa Ukawa wauteka Mkutano Mkuu Chadema

“Kuelekea katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 tutakuwa na wimbo wetu wa pamoja ambao ni ‘bye bye CCM’.”PICHA|MAKTABA


Dar es Salaam. Wenyeviti wenza wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), jana waliuteka Mkutano Mkuu wa Chadema kwa hotuba zilizotoa msimamo wa umoja huo katika mchakato wa Katiba mpya.
Huku wakishangiliwa na wanachama zaidi ya 900 wa Chadema, wenyeviti hao Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), James Mbatia (NCCR-Mageuzi) na Dk Emmanuel Makaidi (NLD) walisema umoja wao hautaishia kudai Katiba mpya iliyotokana na maoni ya wananchi, bali utaendelea hadi katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Ukawa inaundwa na vyama vya Chadema, CUF, DP, NLD na NCCR-Mageuzi.
Viongozi wengine waliozungumza katika mkutano huo ni makamu mwenyekiti wa CCM-Bara, Philip Mangula na msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi.
Wakati wa utambulisho, katibu mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa aliwataja viongozi hao kuwa ni marafiki wa damu huku akimtambulisha Mangula kuwa ni rafiki na mtani wa jadi.
Mbatia
Huku akishangiliwa kila alipotamka neno “people’s power”, Mbatia alianza kwa kuwahoji wanachama wa Chadema, “serikali ngapi?” na kujibiwa “tatu”.
Alisema mkutano huo ni ishara ya Tanzania kuandika historia mpya, hivyo ni lazima iongozwe na viongozi makini huku akiwataka wanachama wa Chadema kutofanya makosa kwa kuchagua viongozi ambao si makini.
“Miaka ya nyuma tulifanya makosa na tuliteleza, ila tukumbuke kuwa makosa ya zamani ni mafundisho yetu ya mbele. Kiongozi mzuri ana sifa tano ambazo ni uwezo wa kupanga hoja, ushirikiano, kuratibu, kutoa maelekezo na kusimamia. Sifa hizo tano Mbowe anazo,” alisema na kushangiliwa kwa nguvu.
Alisema hatua iliyofikia Ukawa ni nzuri, hivyo viongozi wa vyama vinavyounda umoja huo wanatakiwa kuwa makini, kuheshimiana na kuaminiana ili kufikia malengo waliyojiwekea.
“Tanzania ni yetu sote, si ya CCM peke yao na hilo Mangula analijua,” alisema.
Alisema katika mkutano kati ya Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) na Rais Jakaya Kikwete walikubaliana kuwa mchakato wa Katiba mpya usitishwe hadi baada ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2015.

“Tulikubaliana kufanya marekebisho katika sheria na Katiba ya sasa kuhusu tume huru ya uchaguzi, matokeo ya Rais kuhojiwa mahakamani, kuruhusu mgombea binafsi na mshindi atangazwe baada ya kuchaguliwa kwa zaidi ya asilimia 50 ya waliopiga kura.
“Pia tumekubaliana kuwa msingi wa Rasimu ya Katiba uheshimiwe. Pamoja na hayo Bunge la Katiba bado linaendelea, huu ni sawa na ufisadi. Uamuzi kuhusu mchakato wa Katiba utakaotolewa katika mkutano huu tutauheshimu?”
Mbatia alisema Chadema ni chama kikuu cha upinzani Tanzania Bara kama ilivyo kwa CUF Zanzibar, hivyo akavitaka vyama hivyo kukaa meza moja na CCM kuzungumza na kukubaliana kwa masilahi ya Watanzania, “Msionyeshane ubabe baina yenu. Hatuwezi kukubali watu wahuni waharibu Taifa letu.”
Profesa Lipumba
Huku akitumia maneno ya utani na mafumbo, Profesa Lipumba alisema: “Kuelekea katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 tutakuwa na wimbo wetu wa pamoja ambao ni ‘bye bye CCM’.”
Alisema kukwama kwa mchakato wa Katiba kunatokana na wazo la kuandika Katiba mpya lililotolewa na Rais Kikwete kutokuwamo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
“Rasimu ya Katiba ina misingi ya uwajibikaji na wenzetu (CCM) kwa kulitambua hilo wameamua kuinyonga na kuweka mambo yao kwa ajili ya ulaji,” alisema. Alilaani kitendo cha Bunge la Katiba kuendelea na vikao vyake wakati tayari Ukawa kupitia TCD wameshakubaliana na Rais kuwa viahirishwe.
Kuhusu Uchaguzi Mkuu wa 2015, Profesa Lipumba alisema: “Sasa ni muhimu vyama vinavyounda Ukawa vifanye mkutano mkuu wa kupendekeza nani atakuwa mgombea urais.”
Dk Makaidi
Alisema, “Ukawa ni tumaini la Watanzania. Kama ni kuogelea tutaogelea pamoja na ikiwa ni kuzama basi tutazama pamoja.”
Huku akizungumza kwa msisitizo na ushawishi, Dk Makaidi alisema Watanzania wanasubiri kwa hamu maazimio ya Chadema katika mkutano huo, huku akikitaka chama hicho kuhakikisha kinatoa maazimio ya maana. “... suala la Katiba mpya lipo njiapanda na hatujui huko mbele tutakwenda vipi. Tunataka kusikia maazimio yatakayoleta matumaini kwa Watanzania,” alisema.

Mangula
Kwa upande wake, Mangula aliyemwakilisha mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete alisema siasa siyo chuki wala ugomvi, bali ni tofauti za kisera, kiitikadi na kifalsafa na kusisitiza kuwa utaratibu wa vyama vya siasa kukutana mara kwa mara utawaweka karibu zaidi.
Alisema: “Tunapokutana tunajenga utaratibu wa kuvumiliana kisiasa na tuweke nchi mbele na vyama baadaye. Siasa ni kukubali kupokea mawazo tofauti ya mwenzako.”
alisema. na hata mimi (Mangula) nakubali hilo,” alisema.
Alisema tofauti za kisiasa zisiwe chanzo cha viongozi kujenga chuki, “Tuwe kama mashabiki wa Simba na Yanga ambao wanakuwa na upinzani uwanjani, lakini mchezo ukimalizika kila mtu anaendelea na shughuli zake.”
Alisema amejifunza kitu katika mkutano huo akisema ni hamasa, wingi wa watu na jinsi chama hicho kinavyopeleka demokrasia mbele tofauti na mikutano mingine ya awali ya vyama vingine.
Jaji Mutungi
Katika hotuba yake fupi, Jaji Mutungi ambaye alishangiliwa kwa nguvu kutokana na kauli yake ya hivi karibuni kuhusu kutotambua mabadiliko ya Katiba ya Chadema, alisisitiza umuhimu wa demokrasia ndani ya vyama vya siasa na kuvitaka vizingatie amani.
“Utulivu ambao mmeuonyesha leo katika uchaguzi huu uendelee kuwa hivi hata baada ya kumalizika na hata katika ngazi za chini.”
Sheikh atoa mpya
Alipopewa nafasi ya kuomba dua kabla ya kuanza kwa mkutano huo, Sheikh Rajabu Katimba wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, pamoja na dua hiyo, alisema sasa umefikia wakati wa kuiondoa CCM madarakani kwa maelezo kuwa tangu nchi ipate uhuru chama hicho kimeshindwa kuiletea nchi maendeleo.

0 comments:

Post a Comment