Plus 255 Studios

Plus 255 Studios
Home » » MCHAKATO WA KATIBA MPYA: NI ZAIDI YA ZAWADI KWA WATANZANIA

MCHAKATO WA KATIBA MPYA: NI ZAIDI YA ZAWADI KWA WATANZANIA


Dhamira njema na safi ya kupata Katiba aliyokuwa nayo Rais Jakaya Kikwete ilikuwa itupatie Katiba Mpya kwa watanzania katika Mwaka 2014. Dhamira hii ilitafsirika katika Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ambayo sote ni mashahidi iliandaliwa kwa kuzingatia maslahi mapana ya makundi yote na umma wa watanzania.

Msingi mkuu wakati wa kuandikwa kwa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ilikuwa majadiliano yenye staha na ustaarabu, maridhiano na zaidi muafaka miongoni mwa wadau na Taifa kwa ujumla.

Sote tu mashuhuda, Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyoundwa baada ya mchakato shirikishi na uliojikita katika majadiliano, maridhiano na muafaka, ilifanya kazi zake kwa weledi mkubwa, uzalendo wa hali ya juu na kwa kuweka maslahi ya Taifa mbele.

Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilikusanya maoni ya wananchi na sote tu mashahidi nchini kote. Maoni ya wananchi yalikusanywa katika sehemu za wazi ambako wananchi walihamasishwa kutoa maoni yao kwa uhuru na uwazi.

Hata awamu ya kwanza ilipokwisha na Rasimu ya awali kutolewa sote tulithibitisha kwamba kwa hakika maoni ya wananchi yalipewa uzito uliostahili katika Rasimu hiyo. Awamu ya pili, iliyohusisha Mabaraza ya Katiba ya aina mbili, yale yaliyosimamiwa na Tume katika ngazi ya Wilaya na Serikali za Mitaa, na yale yaliyojisimamia yenyewe na kuendeshwa na Taasisi mbalimbali.

Ni kwa bahati mbaya Mabaraza ya Katiba yaliyosimamiwa na Tume yalighubikwa na mashinikizo kutoka vyama vya siasa na hasa Chama cha Mapinduzi. Kitendo hiki hakikuondoa ukweli kwamba Mabaraza ya Katiba ya Taasisi zaidi ya 600 yalitoa maoni yao kwa uhuru na yalikuwa na hadhi sawa nay ale yaliyosimamiwa na Tume.

Hata baada ya awamu ya pili kukamili Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilikuja na Rasimu ya Katiba Mpya Toleo la Pili ambayo bado ilikuwa imeakisi maoni, matakwa, matarajio na ndoto za watanzania wanaopenda kuona Taifa lao linajizaa upya kwa kupata Katiba Mpya kweli kweli itakayojibu changamoto zao.

TUMAINI LA WATANZANIA LINALOPOTEA

Nitarudia kusoma sote tu mashahidi kwamba awamu wa tatu ya Mchakato wa Katiba Mpya imegubikwa na misimamo na maslahi binafsi ya vyama vya siasa na kusahau maoni ya wananchi yaliwasilishwa katika Bunge Maalumu la Katiba kupitia Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inalitaka Bunge Maalumu kujadili Rasimu ya Katiba Mpya na Maudhui yake kama iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Ni bahati mbaya tena kwamba, Rasimu ya Katiba Mpya imewekwa kando na mjadala wa katika Bunge Maalumu umejikita katika Mapendekezo ambayo hayamo katika Rasimu. Hali hii inapoteza uhalali wa Bunge Maalumu la Katiba, si tu kwakuwa linakwenda kinyume na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kifungu cha 25 lakini kwasababu linakwenda kinyume na Matakwa ya wananchi ambayo kwa ujumla wao yako katika Rasimu ya Katiba Mpya iliyowasilishwa na Tume.

Ni bahati mbaya kwamba baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba hasa kutoka kundi la walio wengi wamejivika jukumu lililokuwa la Tume ya Mabadiliko ya Katiba wakidai kupokea maoni mbadala ya wananchi, kitendo hiki ni kinyume na Sheria na ukiukwaji wa kiasi kikubwa wa haki ya wananchi ambao kwa ujumla wao walitoa maoni yao kwa Tume ya Katiba.

Sote tumeshuhudia maoni ya wananchi yaliyo wasilishwa katika Rasimu ya Katiba Mpya yakitupiliwa mbali, na Bunge Maalumu hasa na kundi la walio wengi. Kitendo cha kupuuza maoni ya wananchi hakivumiliki. Bunge Maalumu limegubikwa na vijembe, matusi na kubeza wote wanaosimamia maoni ya wananchi kama yalivyo katika Rasimu ya Katiba Mpya.

Kitendo cha kupuuzwa, kubezwa, kutukanwa na kukiuka Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwa kutojadili Rasimu ya Katiba Mpya na kuleta katika Bunge Maalumu Maoni yasiyokuwemo katika Rasimu, kimepelekea vyama vya Siasa vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na DP kutoka nje ya Bunge Maalumu.

Uamuzi huu hautorudi nyuma mpaka pale maoni ya wananchi yatakapojadiliwa katika Bunge Maalumu, mpaka pale vikao vya bunge maalumu la Katiba vitakapoendeshwa kwa kuzingatia majadiliano yenye staha na ustaarabu, maridhiano na kujenga muafaka wa kitaifa.

KUUTAZAMA MCHAKATO WA KATIBA KWA MACHO YA UCHAGUZI WA 2015

Nchi yetu inapaswa kuingia katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani Mwaka 2015. Ndoto ya watanzania ilikuwa kutumia Katiba Mpya katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015.

Kitendo cha vyama vya siasa kuweka masilahi binafsi katika Mchakato wa kupata Katiba Mpya kama mtaji na maandalizi ya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2015 hakiwatendei haki watanzania. Kitendo cha kuweka mbele masilahi ya vyama hasa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka kesho na kupuuza ndoto za watanzania za miaka 50 ijayo si kitendo cha kizalendo hata kidogo.

Wakati huu wa kuandikwa kwa Katiba Mpya ni fursa kwa watanzania kulipanga Taifa lao kuelekea miaka zaidi ya 50 ijayo na sio kukidhi haja na maslahi ya kundi fulani la watu wachache wasio na mapenzi mema na Taifa hili kutoka chama fulani cha siasa.
Bado hatujachelewa na kama kuna dhamira ya dhati, kujadili Rasimu na Maudhui yake na kuiboresha na si kuleta mambo mapya. Tukapata Katiba Mpya ambayo bado inaweza kutumika kuendesha Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015. Tukiweza kufanya hivyo historia itatukumbuka kwamba tuliliweka Taifa Mbele na tukaweka historia duniani kuwa ndio Taifa ambali limeweza kuandika Katiba katika amani na katika muda mfupi.

MWAKA 2015 BILA KATIBA MPYA: ATHARI ZAKE

Kama tutakwenda katika uchaguzi mkuu wa Mwakani bila Katiba Mpya tutaliingiza Taifa katika “Constitutional crisis”. Katiba inayotumika sasa, Katiba ya Mwaka 1977, ina mapungufu mengi na haiwezi kutupatia uchaguzi ulio huru na wa haki. Hatuwezi kuendelea kufanya Marekebisho ya Katiba wakati Msingi wa Mkuu wa Katiba yenyewe si imara na thabiti.

Tukienda katika Uchaguzi Mkuu Mwakani bila Katiba Mpya tutakwenda tukiwa tumegawika kama Taifa, hali hii si njema kwa wananchi ambao wametuamini na kutupa dhamana ya kuwaletea muafaka wa kitaifa.

Hatuwezi kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi ambayo haijawekewa vyombo vya kikatiba ambavyo vitahakikisha uhuru wa Tume unalindwa na haki kutendeka

Hatuwezi kwenda kwenye Uchaguzi Mkuu mwakani wakati Matokeo ya Uchaguzi wa Rais hayawezi kuhojiwa Mahakamani

Hatuwezi kwenda katika Uchaguzi Mkuu wa mwakani wakati mifumo ya uchaguzi haiko sawasawa

Hatuwezi kwenda katika uchaguzi mkuu Mwakani wakati hoja ya mgombea huru haijapatiwa majibu.
# source: Humphrey pole pole

0 comments:

Post a Comment